dc.description.abstract | Utafiti huu ulichunguza msuko, usimulizi na matumizi ya lugha katika kazi teule za M. S. Abdulla: Kisima cha Giningi (1968) na Kosa la Bwana Msa (2007). Malengo ya utafiti huu yalikuwa yafuatayo: kudhihirisha aina za misuko katika riwaya teule, kubainisha namna usimulizi ulivyoshughulikiwa katika riwaya teule na kuonyesha matumizi maalum ya kunga za lugha katika riwaya zilizoteuliwa. Utafiti huu ulilenga kujibu maswali yafuatayo: ni misuko ya aina gani ambayo M. S. Abdulla anaitumia katika riwaya zake teule? Usimulizi umeshughulikiwa vipi katika riwaya teule za M. S Abdulla? Na je, M. S. Abdulla anatumia kunga zipi za lugha katika riwaya zake teule? Ili kutimiza malengo ya utafiti huu, tulitumia Nadharia ya Naratolojia na ya Umitindo. Huu ulikuwa ni utafiti wa maktabani. Tulisoma vitabu, makala, majarida na tahakiki mbalimbali pamoja na habari za mitandaoni kuhusu kazi za M. S. Abdulla.Kupitia mbinu ya usomaji na unakili, tuliandika na kunukuu data zote muhimu na kuziainisha kulingana na malengo ya utafiti huu kabla ya kuichanganua na kudhihirisha matokeo ya utafiti kwa njia ya kimaelezo. Utafiti ulidhihirisha ya kuwa, riwaya teule za M. S. Abdulla zinatumia misuko, usimulizi na kunga za lugha kwa njia changamano ili kukuza maudhui na dhamira kwa njia inayombainishia msomaji mtazamo wa mwandishi kuhusu matukio mbalimbali katika jamii ya kazi hizi katika nyakati tofauti zilizolengwa. Utafiti huu umewezesha kueleweka kwa kina kwa riwaya teule za mwandishi huyu na masuala anayoyashughulikia kwa msomaji wa kawaida wa fasihi na pia kuibua mitazamo mpya wa kazi hii kwa mhakiki. | en_US |