Nafasi ya wanawake katika uhifadhi wa mazingira katika riwaya ya Nakuruto : mtazamo wa fasihi ya ufeministi wa kiekolojia
Abstract
Fasihi ya kiekolojia ni uwanja uliochipuka miaka ya 1970 na kuendelea miaka ya 1990
kuchanganua, kuchambua na kuhakiki kazi za kifasihi. Uwanja huu unalenga kuangazia fani na
maudhui katika matawi ya fasihi kiekolojia kama vile ya Kiafrika, Kimarekani na Kifeministi.
Utafiti huu unahusu nafasi ya wanawake katika uhifadhi wa mazingira kwa mtazamo wa fasihi ya
ufeministi wa kiekolojia. Lengo kuu la utafiti huu ni kupambanua mchango wa ufeministi wa
kiekolojia katika fasihi ya Kiswahili. Utafiti huu uliongozwa na madhumuni haya: kubainisha
mchango wa ufeministi wa kiekolojia katika uhifadhi wa mazingira katika riwaya ya Nakuruto;
kupambanua mhusika Nakuruto na mchango anaoutoa katika kukabiliana na uharibifu wa
mazingira; kujadili kwa kina changamoto anazopitia mwanawake katika kuhifadhi mazingira;
kujadili athari za masuala ya kimazingira na jinsi zinavyojitokeza katika riwaya. Nadharia
iliyotumika katika utafiti huu ni nadharia ya Ufeministi wa kiekolojia iliyoasisiwa na mfaransa
Francoise d‘Eaubonne mwaka wa 1974. Nadharia hii ilibuniwa kwa ajili ya kuleta mapinduzi ya
kiekolojia hasa kwa kumzingatia mwanamke. Utafiti huu ulifuata muundo wa uchanganuzi wa
makala ambapo maelezo yetu yaliangazia masuala tata yaliyoko kwenye matini tuele. Makala ya
kimsingi ya utafiti yalikuwa ni riwaya ya Nakuruto ilhali makala ya sekondari yalitokana na
usomaji wa vitabu na makala yaliyohusu mada. Utafiti huu ulibainisha kwamba ufeministi wa
kiekolojia una nafasi ya kuwazindua wanawake ili kuleta ukombozi wa kimazingira. Aidha, utafiti
ulitambua kuwa mhusika Nakuruto aliwazindua wanajamii kupitia kwa elimu na maarifa yake ya
kimazingira, hivyo kusababisha mapinduzi. Utafiti ulitambua kwamba wanawake wanasimangwa,
kutukanwa, kudharauliwa na kudunishwa wanapojihusisha na harakati za utunzaji mazingira.
Mwisho utafiti ulitambua kwamba umaskini, kukauka kwa chemichemi za maji, uskwota,
magonjwa na vifo ni athari zinazosababishwa na uharibu wa mazingira. Utafiti huu ulihitimisha
kwamba mwanamke anastahili kupewa nafasi katika uhifadhi wa mazingira na kwamba, fasihi ya
Kiswahili ina uwezo wa kumulika masuala ya kielokojia kama yanavyojitokeza katika jamii. Kwa
kuwa utafiti huu haukuweza kuchunguza vipengele vyote vya kifasihi mazingira, mtafiti
anapendekeza kwamba utafiti wa baadaye uzingatie mikabala mingine kama vile fasihi mazingira
kieneo, Kiafrika na Kimagharibi, hasa kwa mkondo wa kilinganishi
Citation
Master of Arts in KiswahiliPublisher
University of Nairobi